Wednesday, February 10, 2010

Bunge Leo-Kiwira+Richmond: Unafiki wa kisiasa ama ndio uzalendo wa kisasa?

Natazama na kusikiliza kinachoendelea bungeni sasa hivi mintaarafu kuwasilishwa kwa Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu Kiwira na Richmond kama zilivyowasilishwa na Dr Mwakyembe na Shellukindo.

Ninaweza kuielezea hali hii kwa kukubaliana na msemo wa wahenga kwamba CCM, serikali yake na Bunge linahodhiwa na chama hicho limeamua kufanya kinachoitwa ‘funika kombe, mwanaharamu apite’. Watoto wa mjini wanaweza kuelezea hali hiyo kuwa ni ‘tumepigwa mchanga wa macho’. Bunge limerejea kule kule kwa kuwa kama mchezo wa kuigiza kwa kuruhusu usanii wa kisiasa wa serikali; kipeo cha juu cha unafiki wa wanadamu.

Kamati umeshatangaza kwamba imeshaliza kazi yake, Bunge nalo litangaze kufunga huo mjadala kwa bunge zima badala yake sasa ufuatiliaji uachwe kwa kamati za kisekta. Kwa hiyo sasa ripoti za utekelezaji zitapelekwa kwenye kamati za kisekta kwa kuwa kamati husika imesharidhika mpaka sasa kwa utekelezaji ambao serikali imefanya mpaka sasa.

Wakati Kamati ikiyasema hayo inasema kuhusu Kiwira kuwa inaendelea kumshauri CAG afanye ukaguzi kuhusu bilioni 17 zilizoingizwa na serikali kwenye kiwira .(Tujiulize, muda gani agizo hili lilitoka? Kwanini mpaka sasa ukaguzi haujafanyika). Kwa maneno mengine, baada ya serikali kuamua kuuchukua upya mgodi, tuhuma za ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka za kina Mkapa, Yona na wenzao sasa sinaelekea kufunikwa kwa nguvu zote.

Usanii mkubwa zaidi unajidhihirisha kwenye sakata zima la Richmond, ambayo mitambo yake dada ya Dowans ipo mpaka sasa hapa jimboni ubungo. Zikitafutwa kila namna za kuingiza mitambo husika kwenye mkondo wa kuhudumia na kulipwa na serikali ya Tanzania.

Kamati inakiri kwamba ni kweli kuna double payment kwenye ulipwaji wa dola milioni tatu kwa kampuni ya Dowans, kamati inasema tu kwamba inaishauri serikali hizo fedha zirudishwe. (Toka kwa kampuni ya Dowans- ambayo kama ilivyo kwa Richmond inaonyesha kwamba ni kampuni hewa, uhalali wa usajili wake una mushkeli mkubwa). Kamati inatamka kwamba watendaji husika mamlaka zao za kinidhamu zimeona hawana hatia. Kamati inasema viongozi wa kisiasa wakina Msabaha, Karamagi nk uchunguzi wa ndani kuhusu ushiriki wao kwa ajili ya kuwajibishwa umeshakamilika, lakini sasa serikali imeanza uchunguzi wa nje wa kimataifa unaendelea. Kamati inatamka kwamba sasa suala hili likikamilika lipelekwa kwa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje na Usalama( Sasa sio Bungeni tena). Ajabu sana! Suala hili lilianza mwaka 2007; maazimio ya Bunge ni kujiuzulu kwa Lowassa ilikuwa 2008; mpaka leo uchunguzi unaendelea.

Kituko kikubwa zaidi ni hitimisho la Kamati, kwamba kuhusu kumwajibisha Mkurugenzi wa TAKUKURU Hosea kwa TAKUKURU(Wakati huo TAKURU) kuisafisha Richmond; kwamba kamati haiwezi kulizungumzia tena suala hilo na wala haitarajii bunge ilizungumzie kwa kuwa Hosea naye anawachunguza wa bunge(rejea tuhuma kuhusu posho mbili). Hivyo kamati inasema suala hili sasa inaachiwa mamlaka ya juu zaidi(Soma Rais Kikwete). Ningeweza kuchambua azimio moja baada ya lingine katika ya maazimio 13 ambayo yalibaki kabla ya 23 (Hata yale 10 mengine yalikuwa mchanga wa macho).

Lakini yatosha kusema kwamba suala hili ni ishara kwamba sasa makundi ndani ya CCM (lile linalojiita la wapambanaji dhidi ya ufisadi na lile linaloitwa la mafisadi) yanakaribiana kufunika tofauti zao kwa maslahi ya chama chao na utawala wao tunapoelekea uchaguzi wa mwaka 2010 ama pengine huo ndio uzalendo?. Inaonyesha kamati ya chama (party caucus) imefanya kazi yake kwa kile kinachoitwa ‘kuchukua maamuzi magumu (soma mabovu/bomu). !. Hii inaweza kutoa ishara kuhusu nini kitatokea kwenye ripoti ya Kamati ya Mwinyi na mwelekeo wa chama hicho tawala kwa ujumla. Haya ni madhara ya kuwa na hodhi (dominance/monopoly) ya chama kimoja bungeni.

Hii ni changamoto kwa umma tunapoelekea katika uchaguzi mkuu. Tukumbuke maneno ambayo CHADEMA tuliyasema mwaka 2005; Kwamba mabadiliko ya kweli katika taifa letu, hayawezi kuletwa na mafisadi wale wale, wa chama kile kile, chenye uoza ule ule, wakiendeleza yale yale kwa Ari, nguvu na Kasi mpya. Kwa falsafa ya chukua chako mapema(ccm), Tanzania yenye neema haiwezekani. Tuunganishe nguvu ya umma kuchagua viongozi mbadala wenye dira na uadilifu tuweze kujenga taifa lenye uwajibikaji kwa kubadili mfumo wa utawala; mabadiliko ya kweli yanawezekana. Tuwe wakala wa mabadiliko tunayotaka kuyaona; Mwenyezi Mungu atuwezeshe kufika salama.





1 comment:

ray05 said...

kaka kwa kweli tumechoshwa na siasa ya Tanzania.Chama kinaongoza bunge na bunge linaongoza serikali.
mi naona suluhisho pekee ni kuongeza idadi ya wabunge wa upinzani bungeni na tena sio wabunge kwa sababu tu ni wa upinzani,bali wenye uchungu na malengo na nchi yetu.ni muda sasa wa kuamka na kuachana na siasa za kinafki.TUMEICHOKA CCM