Sunday, February 27, 2011

Taarifa fupi ya ukaguzi wa uendeshaji wa mradi wa maji Goba

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ameitisha mkutano wa wananchi wa kata ya Goba utakayofanyika eneo la Goba mwisho mwembemadole siku ya jumapili tarehe 27 Februari 2011 kuanzia saa 9 alasiri mpaka sasa 12 jioni.

Mkutano huo utajadili ajenda mahususi za maendeleo kuhusu maji, barabara na ulinzi. Hata hivyo, inatarajiwa kwamba ajenda ya maji itachukua uzito mkubwa katika mkutano huo kutokana na malalamiko mbalimbali ambayo yamewasilishwa kwa ofisi ya mbunge na wananchi mbalimbali.

Katika Mkutano huo Mbunge wa Ubungo anatarajiwa kutoa fursa ya ripoti ya ukaguzi kuwekwa hadharani ripoti ambayo haikutolewa kwa wananchi toka mwaka 2007 ukaguzi ulipokamilika.
Itakumbukwa kwamba kwa kipindi cha miaka takribani mitano pamekuwa na malalamiko kuhusu maji yakihusisha pia tuhuma mbalimbali kuhusu mradi wa maji. Kutokana na hali hiyo tarehe 21 Oktoba 2007 palifanyika mkutano wa wananchi ambapo pamoja na mambo mengine iliazimiwa kwamba kamati iliyokuwa ikihusika na mradi wa maji isimamishwe kwa muda kuruhusu ukaguzi wa uendeshaji wa mradi.

Kutokana na uamuzi huu wananchi waliunda kamati ya muda ya kupitia uendeshaji wa mradi na kuwasilisha mapendekezo yake kwa uongozi na wananchi kabla ya tarehe 27 Oktoba 2007.
Kamati hiyo ilipewa majukumu kadhaa ikiwemo: Kupitia mahesabu na mfumo wa uendeshaji wa mradi kwa msaada wa ushauri wa kitaalamu kutoka kwa mkaguzi wa Manispaa (auditor) ili kutoa maoni juu ya madhaifu, mfumo na/au namna bora na endelevu ya kuuendesha mradi huu na Kuwasilisha mapendekezo kwa timu ya uongozi na wananchi ili kutoa fursa ya majadiliano na maamuzi katika mkutano uliopendekezwa kuwa tarehe 27 Oktoba 2007.

Hata hivyo, pamoja na ukaguzi husika kukamilika toka mwaka 2007 mkutano wa wananchi haukuitishwa katika tarehe husika wala tarehe nyingine yoyote katika kipindi cha miaka zaidi ya mitatu mpaka hivi sasa wala ripoti husika haijawahi kutolewa hadharani.

Hivyo, Mbunge mpya wa Ubungo ameamua kuitoa ripoti hiyo hadharani kupitia mkutano na wananchi pamoja na mtandao kama ifuatavyo ili mjadala uweze kufanyika ili kukubaliana hatua za kuchukua katika mazingira ya sasa mwaka 2011:


TAARIFA FUPI YA UKAGUZI WA UENDESHAJI MRADI WA MAJI GOBA

1.0 Utangulizi:

Tarehe 21 Octoba 2007 wananchi wa Kata ya Goba Manispaa ya Kinondoni Mkoani Dar re Salaam walishiriki katika mkutano wa mashauriano na viongozi mbalimbali wa Kata na Mbunge wao (Jimbo la Ubungo) Mh. Charles Keenja. Mkutano huu uliitishwa na Mh. Kisoky ,Diwani wa Kata ya Goba kama sehemu ya kufuatilia maagizo na ushauri wa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni kufuatia malalamiko ya matatizo ya maji yaliyokuwa yamefikishwa ofisini kwake na baadhi ya wananchi. Mh. Diwani aliwaalika pia viongozi watendaji wa Kata ya Goba pamoja na wa mitaa yote minne ya Kinzudi, Goba, Kulangwa na Matosa. Pamoja na kwamba wananchi kwa ujumla walikuwa na mambo kadhaa na ambayo Mh. Mbunge Keenja alipata fursa ya kufafanua na kuyatolea majibu, agenda kubwa ilikuwa ni kukatiwa maji na DAWASCO kutokana na kulimbikiza deni linalofikia shillingi millioni kumi na tano (TZS 15,000,000)

Kufuatia malalamiko na manung’uniko toka kwa wananchi zikiwepo tuhuma za ubadhirifu ilionekana ni hekima kuisimamisha kwa muda kamati hii ili kuruhusu ukaguzi wa uendeshaji wa mradi. Kwa maana hii uongozi kwa pamoja na wananchi watakuwa wameshiriki kwa vitendo kusimamia utawala bora badala ya kutuhumu bila uthibitisho. Kwa upande mwingine wajumbe wa kamati ya mradi wa maji watapata nafasi ya kujibu hoja mbalimbali zitakazoibuliwa na ukaguzi huu. Kutokana na uamuzi huu wananchi walipendekeza kamati ya muda ya kupitia uendeshaji wa mradi na kuwasilisha mapendekezo yake kwa uongozi na wananchi kabla ya tarehe 27 Octoba 2007. Kamati hii ilitakiwa kufanya mambo matatu;

I. Kushirikiana na Mh. Mbunge na Diwani kupata/kukopa fedha kiasi cha millioni nne (TZS 4,000,000) kulipia sehemu ya deni la TSZ millioni kumi na tano (15,000,000) kama sharti la Dawasco kuirejesha mita ya maji pale Tangi bovu kwenye kianzio au muunganisho na bomba kubwa;
II. Kupitia mahesabu na mfumo wa uendeshaji wa mradi kwa msaada wa ushauri wa kitaalamu kutoka kwa mkaguzi wa Manispaa (auditor) ili kutoa maoni juu ya madhaifu, mfumo na/au namna bora na endelevu ya kuuendesha mradi huu,
III. Kuwasilisha mapendekezo kwa timu ya uongozi na wananchi ili kutoa fursa ya majadiliano na maamuzi katika mkutano uliopendekezwa kuwa tarehe 27 October, 2007.

1.1 Wajumbe wa Kamati waliopendekezwa ni hawa wafuatao:
I. Ndugu Ibrahim Mabewa –Mtendaji wa Kata ya Goba (Mwenyekiti)
II. Ndugu Emanuel Meso Chacha -Mjumbe/Katibu
III. Ndugu Hamisi Deule –Mjumbe
IV. Ndugu Mama Mwazani Ramadhani- Mjumbe
V. Ndugu Willy Muro Mjumbe-Mtaalamu wa mambo ya fedha na ukaguzi
VI. Auditor toka Manispaa ya Kinondoni ambae Mh. Mbunge angemwomba kwa mkurungenzi – Aliteuliwa jumatatu ya 22octoba 2007- Ndugu Paul Kandokando

Kamati hii ilifanya kazi ilizopangiwa na kuwasilisha taarfia za awali katika kikao cha Mbunge na wananchi kilichofanyika wiki moja baadaye yaani tarehe 27 Octoba 2007. Ikiwa imefanikiwa kutimiza jambo moja muhimu la kuunganishiwa maji na DAWASCO kamati iongezewe nguvu za utendaji ili iweze kumalizia kwa haraka majukumu yaliyosalia na kuyatolea taarifa katika mkutano wa wananchi ambao ungeitishwa baadaye. Mh. Mbunge aliwasihi wananchi waendelee kuwa na subira na alikuwa anawahi kikao cha Bunge mjini Dodoma. Wananchi walipendekeza wajumbe wafuatao kuongezwa kwenye kamati ili kuharakisha mategemeo na makusudio ya kuwa na mradi endelevu. Wajumbe walioongezwa na mitaa wanayotoka kwenye mabano ni hawa wafuatao

VII. Mama Rose Basaka (Mjumbe- Kizundi)
VIII. Ndugu Rwegasira (Mjumbe-Kinzudi
IX. Maulidi Selemani –(Mjumbe-Goba)
X. Mama Mnandi(Mjumbe-Goba)
XI. Ndugu Wambura –(Mjumbe-Kulangwa)


2.0 Matokeo na Taarifa ya Ufuatiliaji na Ukaguzi:

2.1 Kulipia na Kuunganishiwa Mita na Dawasco
Tunasihi kwa niaba ya wananchi tumshukuru Mh. Mbunge Keenja akishirikiana na diwani kwa jitihada kubwa walizofanya kupata mkopo wa shillingi millioni nne (4,000,000) toka Manispaa ambapo iliwezesha kulipa sehemu ya deni siku moja tuu baada ya kikao cha jumapili;

2.2 Ukaguzi wa Mfumo (systems audit), Utendaji (Performance audit) na Utawala wa fedha (Financial audit)

Tarehe 22 October,2007 wajumbe wanne wa kamati wakiongozwa na Mwenyekiti (Mtendaji wa Kata) na Auditor toka Manispaa walikubaliana nini kifanyike kutokana na uharaka wa taarifa, ukubwa wa eneo la mradi kijiografia na mazingira halisi ya ukaguzi. Kamati hii iliafiki kuwa ili kupata matokeo mazuri ya kazi hii yafuatayo yanastahili kufanywa;

2.2.1 Kupata uthibitisho na uwiano wa maji yaliyonunuliwa toka DAWASCO na yale yaliyouzwa kwa wateja kwenye vioski (mabomba ya wananchi) na yale yaliounganishwa majumbani. Malinganisho haya yanatoa fursa ya kubaini upotevu wa bidhaa (yaani maji) kwa njia ya kuvuja (leakages), yanayotumika kuosha ndoo kwenye vituo n.k

2.2.2 Ili kupata uthibitisho huu (2.2.1 hapo) juu ilibidi timu ya ukaguzi ipitie vituo vyote vya wananchi na majumbani na kusoma mita, kupata uthibitisho wa gharama za maji, malipo ya billi n.k.


2.2.3 Kulinganisha taarifa hapo juu (confirming) na taarifa na ripoti za kamati, pamoja na nyingine muhimu zikiwepo za DAWASCO.

2.3 Mfumo na Utendaji
Tulipitia wateja wapatao toka vituo mbalimbali. Sehemu nyingine tuliwakuta wenye nyumba na mahali pengine hatukuwakuta. Kwa sababu hii hatukuweza kupata maelezo muhimu juu ya gharama za kuunganishiwa na ulipaji wa bili ili kupata uthibitisho wa jumla ya fedha iliyopkelewa. Kwa sehemu kubwa tuliweza kulinganisha kiwango kilichotumika na bili za August, Septemba na Octoba 2007 kwa wale waliokuwa nazo. Mahojiano na wateja pamoja wasimamizi wa vituo vya wananchi ni kama yafuatayo;

2.3.1 Malipo ya Ankara za Maji na Utoaji wa Risiti – Idadi kubwa ya wateja tuliowatembelea walikiri kuwa wamekuwa wakilipa gharama za maji kila wanapopewa bili lakini hawakuwa wanapatiwa risiti. Wakati mwingine wakiuliza wanaadiwa kuwasilishiwa baadaye ahadi ambazo hazikutekelezwa. Huu ni udhaifu mkubwa kwa wananchi/wateja kutokujua wajibu wao au tu mwendelezo wa utamaduni wa kupuuzia mambo muhimu. Pale ambapo kamati ilipatiwa bili za mwezi tulijaribu kuona kama kulikuwa na malimbikizo. Hii ni kwa sababu bili inaonyesha salio la kipindi kilichopita na gharama mpya ya mwezi. Bili tulizopitia zinaonyesha kuwa kwa sehemu kubwa wateja walikuwa wanalipa ankara zao kwa wakati.

2.3.2 Kuunganishiwa Maji- Ukaguzi unaonyesha kuwa mfumo wa maombi ya kuunganishiwa maji pamoja na malipo haukuwa na uwazi. Yumkini ndio sababu ya kuunganishiwa maji kwa malipo tofauti. Kutokana na mahojiano na wateja tulishuhudiwa kuwa baadhi wameunganishiwa kwa TZS 160,000, wengine TZS 210,000; TZS 310,000; TZS 500,000 mpaka TZS 700,000.

2.3.3 Usimamizi wa Vituo/Mabomba ya Wananchi – Kila kituo kina watu wanaoitwa kamati ya maji ambapo wajumbe wake husimamia uuzaji wa maji kwa wananchi. Kwa kipindi kirefu ndoo moja ya lita ishirini iliuzwa kwa TZS 40/- hadi hivi karibuni ilipopandishwa na kuwa TZS 50/-. Baada ya mauzo msimamizi wa mradi ndugu Msasa alikuwa anawapitia wauzaji na kukusanya mapato kwa utaratibu tuliouona kuwa ni dhaifu. Baadhi ya wauzaji wana daftari wanazoandikia mapato wakati wengine hawana. Kwa kuwa hakuna leja inayoonyesha kiwango cha maji yaliyouzwa na kwa kwa kuwa hakukuwepo na risiti basi uwezekano wa kuthibitisha mapato kwenye vioski vya wananchi ni mgumu.

Baadhi ya vituo hivi kwa mfano Mbuyuni (Kwa Sanya) havina mita na wananchi wanauiziwa maji kwa utaratibu ambao hatukujua ni kwa vipi waliweza kufahamu kiwango cha maji na fedha zilizopatikana. Baadhi ya mita za kwenye vituo ni mbovu ambapo vingine zilishabadilishwa mara zaidi ya moja lakini hatukuweza kupata mita za zamani. Kwa sababu hii imekuwa vigumu kupata kiwango cha maji kilichouzwa kwa kila kituo.

2.3.4 Mabomba ya Majumbani- Tunashawishika kutokuamini kama baadhi ya wateja si washiriki wa tuhuma wanazoelekeza kwa kamati. Pili tumegundua kuwa wapo watu walounganishiwa katika eneo la Mbezi Juu/Tangi Bovu. Tulikuta baadhi ya nyumba zikiwa na mita mbovu japokuwa wanapata maji. Hatukuweza kutambua bili ya maji inatolewaje wakati mita imeharibika. Baadhi ya Ankara zinatia shaka. Mfano wakati mjumbe mmoja wa kamati alikiri kwenye mkutano wa wiki iliyopita kuwa anacho kisima cha lita 25,000 na amekuwa akiuza maji, mita yake ilionyesha kuwa amechota maji uniti 11 tu sawa na lita 11,000. Kwa tafsiri nyingine hajawahi kuchota maji yonayofikia hata nusu yakisima chake tangu mradi uanze.

Mahali pengine, mteja ambaye amekuwa akiuza maji kwa wingi na kwa muda mrefu eneo la Kunguru mita yake imesoma unit 125 tu. Tunashawishika kuamini kuwa upo utaratibu wa kudivert maji nje ya mfumo wa mita kwani hata kamati iliporudi kwa mteja mwenye unit 11 tulikuta ameshaingoa. Hii ina maana kuwa hata tulipofungulia maji siku ya jumatano yaliyoingia kwake hayana kumbukumbu yeyote.

2.3.5 Usomaji wa Mita Tangi Bovu – Usomaji wa mita kuu tangi bovu ulikusudia kuoanisha na kuthibitisha kama kuna uhusiano kati ya maji yaliyonununuliwa kutoka DAWASCO NA YALE YANAYOONYWESHWA NA ANKARA TULIZOZIPITIA KATIKA Vituo. Kutokana na ukaguzi wetu mita kuu ya Tangi Bovu ilichukuliwa na DAWASCO walipokata maji tarehe 4/octoba/2007 ikiwa inaonyesha matumizi ya mita za ujazo 67,640. Idadi hii ndio inayoonekana kwenye bili ya DAWASCO iliyosainiwa tarehe 22 october 2007 ya mmoja wa wateja. Kiwango hiki cha maji kimeambatanishwa na fedha zilizolipwa na kamati ya maji kuanzia Octoba 2005 na kuonyesha kuwa DAWASCO inadai TZS 15 millioni.

Kamati hii haikuwa na uwezo wa kupitia nyaraka za DAWASCO kuthibitisha kama walikosea au la. Lakini ukaguzi wetu unatia shaka kubwa kutokana na yafuatayo;

Leja iliyopo Tangi Bovu (tumeambatanisha vivuli) ambayo inasainiwa na mlinzi na mwendesha machine Ndugu Mustapha Jumanne inaonyesha kuwa tarehe 5 Decemba mwaka jana (2006) DAWASCO ilikuwa imeuzia mradi wa maji Goba mita za ujazo 38,565.5 kuanzia octoba 2005 ambapo kiwango hiki kilifikia mita za ujazo 67,640. Ukilinganisha na usomaji wa mita majumbani kwa watu walounganishiwa maji na vioski vya wananchi kiwango hiki ni kidogo sana ukilinganisha na matumizi yanayoonyweshwa na mita ambayo yanazidi mita za ujazo 200,000. Hii ni tofauti kubwa ambayo ambayo inahitaji nguvu kubwa zaidi ya kisheria na kiutawala kuichunguza.

Yumkini tofauti kubwa hapo juu yaweza kuwa mita za wateja ni mbovu lakini ni vigumu kuamini kwa nini mteja akubali kuendelea kutumia mita mbovu. Na hata kama akikubali msimamizi wa mradi anampaje bili ya mwezi na yeye analipa kwa utaratibu upi ukizingatia pia kuwa hakuna risiti?


3.0 Majumuisho na Ushauri Wetu

3.1 Mradi haukuendeshwa kwa utashi wa kutosha kuthibitisha kama kulikuwa na nia na dhamiri njema ya kutoa huduma hii muhimu;
3.2 Maji yaliyotumika hayawezi kuwa mengi kuliko yaliyouzwa na DAWASCO. Kuna walakini mkubwa ambao mamlaka husika zinapaswa kuchukua hatua;
3.3 Kuna fununu kuwa wapo watu waliounganishiwa maji kwa siri hasa Tangi Bovu na Sehemu ya Mbezi Juu. Tumekubali fununu kwa kuwa hili ni tatizo sugu linaloikabili DAWASCO na mashirika mengine ya maji ya Miji ya Tanzania.Tusingeweza kukataa kupokea fununu kwa kuwa zinalingana na matatizo sugu yanayotangazwa na vyombo vya habari sehemu mbalimbali. Kamati haikuwa na mamlaka ya kuingia nyumbani kwa watu na kuchimba ili kuthibitisha. Lakini hiki ni kianzio muhimu kwa kamati mpya au ile ya zamani ikiwa ni utashi wa wananchi na viongozi kuirejesha kwenye utendaji.
3.4 Uthibitisho wa Kimazingira (Circumstantial evidence) unaonyesha wapo wananchi waliokula njama (collusion) za kujipatia maji kwa kuyaingiza kwenye visima bila kupitia kwenye mita. Haingii akilini mtu ana visima vikubwa huku akiuzia majirani maji mwaka mzima na mwishowe awe na mita inayosoma ujazo wa mita 125.
3.5 Mfumo wa uuzaji wa maji katika vituo unaashiria ushirikiano usiokuwa wa kiuadilifu kati ya mkusanyaji wa fedha na baadhi ya wauzaji. Ni vigumu kuamini uhusiano wa kiutendaji kwa mtu anayeuza maji kwenye kituo kisichokuwa na mita huku akiendelea kukabidhi chochote alichokipata bila hata ya maandishi huku mpokeaji wa fedha akiwa haitaji uthibitisho zaidi.

3.6 Kwa ujumla mfumo (system), utendaji (performance) na utawala wa fedha (financial management) ulikuwa ni dhaifu sana kiasi ambacho kimoja hakikumsaidia mwenzake. Kwa maana nyingine kulikuwa hakuna mfumo ulioruhusu utendaji mzuri wa kazi na kwa kwa kuwa utendaji ulikuwa dhaifu basi utawala na usimamizi wa fedha uliharibiwa kwa manufaa binafsi au ya kikundi cha watendaji.

3.7 Uwezo wa kuthibitisha kiwango cha ubadhirifu kinahitaji yafuatayo;

3.7.1 Uwepo muda wa kutosha kufuatilia kila mtu aliyeunganishiwa maji atoe taarifa ya fedha yote aliyolipa;
3.7.2 Kamati za maji kwenye vioski vya wananchi wahojiwe kueleza ni kiasi gani na kwa uthibitisho kiasi walichokabidhi kwa mkusanyaji wa fedha;
3.7.3 Uthibitisho toka DAWASCO kama kweli kiwango kinachoonyeshwa kwenye bili yao ni halali. Kama ni halali basi mita zote za wananchi zitakuwa ni mbovu au zimetengenezwa kwa utaratibu tofauti na mfumo wa dunia (international standards) wa kupima matumizi ya maji.
3.7.4 Mamlaka za kiutendaji (administration/government) zenye nguvu za kisheria zipitia bomba lote kuona watu waliounganishiwa maji kwa siri. Kinyume na kutokufanya wananchi maskini wataendelea kulipishwa gharama kubwa kufidia ubadhirifu wa watu wachache, yumkini wenye uwezo mkubwa tu wa fedha.

Taarifa hii imeandikwa na:

1. Imanuel Willy Muro (Mjumbe kamati ya Maji-Goba
2. Paul Kandokando –Auditor wa Manispaa ya Kinondoni

Nov 2007

2 comments:

Castro Pius said...
This comment has been removed by the author.
Castro Pius said...

Greetings,

What has been done by the Ubungo MP, is exectly what is expected by citizens from their laeders.

I have been embarrassed so much with all these what we call poor and ineffectual systems, performance and financial administration.

I think its better to use the few resources we have to invoke capacity building seminars to these watendaji so as to secure our resources from being lost or misapplied.

Also MPs are heads/chairpersons of Constituency Developmet Committee, and they should therefore act proactive enugh to prevent sabotage and squandering of public resources.

Best Regards,

+255 755 640167