Saturday, March 26, 2011

MBUNGE AELEZWA CHANZO CHA WIZI KUIBUKA TENA KATIKA ENEO LA UBUNGO MATAA

Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika ameelezwa chanzo cha kuibuka tena kwa wimbi la wizi katika eneo la Ubungo mataa linalounganisha barabara za Morogoro, Mandela na Sam Nujoma.
Mnyika alielezwa hayo na Diwani wa Kata ya Ubungo Boniface Jacob alipomuita ofisi ya mbunge Jimbo la Ubungo jana (24 Machi 2011) kueleza sababu za kuibuka tena kwa vibaka na waporaji kwenye eneo hilo katika siku za karibuni ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa kudhibiti hali hiyo.

Awali Mnyika aliumueleza Diwani kuwa katika kipindi cha kuanzia mwishoni mwa mwezi Februari na mpaka mwezi Machi amepokea malalamiko toka kwa wananchi wenye magari na wanaotembea kwa miguu katika maeneo hayo kuporwa mali zao katika eneo hilo ambalo vitendo hivyo vilidhibitiwa mwanzoni mwa mwaka 2011 kutokana na ulinzi shirikishi.

Itakumbukwa kwamba katika kipindi cha miaka iliyopita palikuwa na wimbi kubwa la wizi katika eneo hilo ambavyo vilidhibitiwa kuanzia mwishoni mwa mwaka 2010 na mwanzoni mwa mwaka 2011 baada ya kutokea kwa mabadiliko katika kimkakati katika jeshi la polisi na kiungozi wa kisiasa na hivyo kufanya suala la usalama katika eneo hilo kupewa kipaumbele cha ziada.

Kwa upande wa Jeshi la Polisi Kamanda wa Kanda Maalum wa Mkoa wa Dar es salaam Seleman Kova na Kamanda mpya wa polisi Mkoa wa Kinondoni Charles Kenyela waliweka mkazo kwenye ulinzi shiriki ukiungwa mkono na Diwani mpya wa kata ya Ubungo Boniface Jacob na mbunge wa jimbo hilo.

Kama sehemu ya hatua zilizochukuliwa paliundwa kikundi cha vijana wa ulinzi shirikishi ambacho kilipatiwa vifaa na wadau na kuanza kazi ya kushirikiana na jeshi la polisi na hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa vitendo vya wizi katika eneo hilo hususani katika kipindi cha mwezi Januari mpaka Februari 2011.

Diwani Boniface Jacob alimueleza mbunge kwamba chanzo cha kuibuka kwa hali hiyo ni vitendo vinavyofanywa na baadhi ya askari polisi wasiowaaminifu ambao kwa miaka kadhaa walikuwa wakishirikiana na wezi kuanza tena kuuhujumu mfumo wa ulinzi shirikishi uliowekwa kwa kuwakamata vijana ambao walikuwa wakifanya ulinzi katika eneo hilo na hivyo kuwaacha vibaka na waporaji kurejea katika eneo hilo kwa kuwa wanahongwa mgawo.

Mnyika alimuelekeza Diwani kukutana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni Charles Kenyela kumweleza kwa kina suala hilo hili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa na jeshi hilo kuhakikisha usalama wa raia katika eneo hilo hususani nyakati za jioni.

“ Kwa kuwa sasa niko katika jukumu la kuwawakilisha wananchi kwenye vikao vya kamati ya nishati na madini ya bunge vinavyoendelea hivi sasa, niwakilishe katika kukutana na uongozi wa jeshi la polisi. Na usisite kuwataja kwa majina askari wanaotuhumiwa kushirikiana na wezi toka maeneo ya nje ya kata ya Ubungo kuja kufanya wizi katika eneo letu ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kulinda usalama wa wananchi na mali zao”, Alisema Mnyika.

No comments: