Sunday, June 19, 2011

Majibu kwa Maswali yenu kuhusu POSHO

Kutokana na maswali ya mara kwa mara toka kwa wananchi kupiti mtandao na simu ya mkononi kutaka kujua msimamo wangu kuhusu mjadala wa posho unaoendelea hivi sasa. Naomba niwakumbushe tu kwamba msimamo wangu nimekuwa nikiuweka bayana kuanzia kampeni za mwaka 2005 na hata za mwaka 2010; ambapo nimekuwa nikiahidi kwamba nikichaguliwa nitataka mabadiliko katika mfumo wa posho na mishahara ya wafanyakazi.
Nimekuwa nikieleza bayana kwamba siridhishwi na pengo la mishahara katika utumishi wa umma kati ya kima cha chini na kima cha juu, na niliahidi kwamba wakati nikiendelea kutaka mabadiliko katika mfumo wa mishahara na kuboreshwa kwa mishahara ya watumishi wa umma binafsi nitaonyesha mfano kwa kukata asilimia 20 ya mshahara kuelekeza katika kuchangia masuala ya elimu jimboni. Aidha, nimekuwa nikikosoa mfumo wa malipo ya posho za vikao (Sitting Allowance) na kutaka ubadilishwe na kama sehemu ya kutaka mabadiliko hayo nilitangaza hadharani kuelekeza posho hiyo katika masuala mbalimbali ya maendeleo. Kauli zangu hizo zimewahi kunukuliwa na vyombo kadhaa vya habari kwa nyakati mbalimbali. Nashukuru pia msimamo huu pia ni msimamo rasmi wa chama uliopo pia kwenye Ilani ya Chama ya Uchaguzi Mkuu 2010.

Mara baada ya kuchaguliwa nimekuwa nikitekeleza ahadi hiyo kwa kutoa asilimia 20 ya mshahara kuchangia elimu jimboni kupitia ofisi ya mbunge na Taasisi ya Maendeleo Ubungo (Ubungo Development Initiative). Nimekuwa pia nikizielekeza fedha hizo za posho ya vikao (Sitting Allowance) kwenye masuala ya kimaendeleo jimboni ikiwemo ya kuchangia mipango ya maji ya wananchi katika baadhi ya mitaa.

Na iwapo Serikali itaacha kuzifuta posho hizo kwenye mwaka huu wa fedha nitawasiliana na ofisi ya bunge kuweka utaratibu rasmi zaidi wa fedha hizo kuelekezwa moja kwa moja katika miradi ya maendeleo jimboni Ubungo hususani kupitia CDCF (ingawaje naungana na wanaharakati kupinga mfuko huo); lakini nitazingatia pia makubaliano ya pamoja kuhusu suala husika katika chama. Kabla ya kubadilishwa kwa mfumo mzima wa posho si jambo lenye maslahi ya umma kuziachia posho hizo zikatumiwa kiubadhirifu na serikali inayoongozwa na CCM badala yake ni lazima kuweka mazingira ya kuhakikisha fedha hizo zinatumika kwenye masuala ya kimaendeleo kinyume na hapo itakuwa ni sawa sawa na ‘kumsusia fisi bucha’. Nilichukua pia msimamo kama huo kwenye suala la mikopo ya magari ya wabunge, wakati wa kampeni nilipinga kiwango cha mikopo kinachotolewa cha milioni 90 kwa ajili ya gari kuwa ni kikubwa; na baada ya kuchaguliwa nilipewa mkopo huo na kuupokea. Hata hivyo, niliendelea na msimamo wa kutonunua gari la milioni 90 na badala yake sehemu ya mkopo huo niliuelekeza kwenye mfumo wa kutoa mikopo kwa madiwani wa jimbo la Ubungo kwa ajili ya kazi zao. Naamini kwamba madiwani wanapaswa kuwekewa utaratibu bora zaidi wa kuwezesha utumishi wao; wakati tukiendelea kusukuma ajenda pana zaidi ya kuongeza mamlaka ya serikali za mitaa na uwajibikaji katika halmashauri niliona nianze kwa kuongeza ufanisi na madiwani wa jimbo letu kwa njia mbalimbali ikiwemo mfumo huo wa mikopo.

John Mnyika (Mb)

1 comment:

Anonymous said...

hii ni isharaa ya uongozi bora... keep it up brother..