Friday, November 25, 2011

Juu ya hoja ya kutaka kupandishwa bei ya umeme!

Mnyika ataka bei ya umeme isipandishwe
Wednesday, 23 November 2011

MBUNGE wa Ubungo,jijini Dar es Salaam, John Mnyika, ameitaka Serikali kusitisha ombi la Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), kupandisha bei ya umeme kwa asilimia 155, ili kuepusha athari katika usalama na uchumi wa nchi, utakaozidishwa na mfumuko wa bei.


Mbunge huyo alisema hayo jana kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari, kufuatia hatua ya Tanesco kutaka kupandisha bei ya umeme kwa kiwango hicho.

Mnyika alisema Serikali inapaswa kuchukua hatua za haraka kuinusuru Tanesco dhidi ya mzigo mkubwa wa gharama unaoikabili, badala ya upandisha bei ya umeme kwa wananchi.

"Itakumbukwa kwamba Novemba 9 mwaka huu Mamlamka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), ilipokea ombi la dharura kutoka Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) la kuidhinisha ongezeko la bei za huduma ya umeme kwa wastani wa asilimia 155 ya bei ya sasa, bei ambayo ni zaidi ya mara tatu ya sasa" alisema Mnyika.

Mnyika pia alisema ni muhimu kwa wananchi kushiriki kwa wingi katika mkutano wa kukusanya maoni ya wadau ulioitishwa na Ewura kuhusu upandishaji bei ya umeme ili nao, wapate fursa ya kutoa maoni yao ipasavyo.


"Wananchi wakumbuke kwamba hii ni mara ya pili katika kipindi cha takribani mwaka mmoja kwa Tanesco kupandisha bei ya umeme. Mara ya kwanza ilikuwa Januari mwaka huu ambapo umeme ulipanda kwa asilimia 18.5 na kuchangia katika kupanda kwa gharama za uzalishaji na kuongeza ugumu wa maisha kwa wananchi" alisema.

Mnyika alisema kabla ya kuongeza bei ya umeme kwa wananchi, Serikali inapaswa kwanza kuwaeleza namna ilivyowapunguzia mzigo kwa kupitia upya mikataba inayoinyonya Tanesco.

Alisema uamuzi wa kupandisha bei ya umeme utasababisha ongezeko la mfumuko wa bei , jambo ambalo litatishia usalama na uchumi wa nchi na maisha ya wananchi kwa jumla.

“ Serikali izingatie kwamba mfumuko wa bei nchini hivi sasa umefikia asilimia 17.9 na bidhaa zinazochangia mfumuko huo kwa kiwango kikubwa ni vyakula, mafuta na umeme. Kupanda kwa ya nishati ya umeme pekee kumekuwa kwa asilimia 37.4 na kusababisha kupanda kwa gharama za maisha” alisema.

Alisema mpango huo wa kupandisha bei ya umeme kwa wastani wa asilimia 155 unapaswa kusitishwa ama kubadilishwa kwa kulinda maslahi ya makundi mbalimbali kwa kuzingatia aina za matumizi.

Chanzo: http://www.mwananchi.co.tz/habari/51-habari-nyingine/17784-mnyika-ataka-bei-ya-umeme-isipandishwe

No comments: