Monday, February 27, 2012

Hatimaye Ujenzi wa Choo cha Kituo cha Mabasi Mbezi Luis Waanza

Jana tarehe 27 Februari 2012 nimefuatilia tena kwa mamlaka husika na kujulishwa kwamba tayari ujenzi wa choo na uzio umeshaanza na kwamba sasa unafanywa na fedha za umma toka TANROADS badala ya Manispaa ya Kinondoni.

Mtakumbuka kuwa mwezi Januari 2012 nilifuatilia kwa nyakati na namna mbalimbali kutaka ujenzi wa choo katika Kituo cha Daladala cha Mbezi Luis uharakishwe. Nimefanya hivyo pamoja na kutambua kwamba kituo husika kimejengwa katika eneo la hifadhi ya barabara (nitachukua hatua zingine kuhusu hili), kinaweza kutumika kwa miaka kadhaa kupunguza msongamano wa magari.

Kwa kuwa kazi ya mbunge ni kuwakilisha wananchi na kuisimamia serikali nilizihoji mamlaka husika ambazo ni TANROADS na Manispaa ya Kinondoni ambazo zilikuwa zirushiana mpira kuhusu ujenzi wa choo. Hatimaye nilijulishwa kupitia bodi ya barabara na RCC kuhusu choo kitajengwa na Manispaa ambayo haikuwa imetenga bajeti husika.

Nilikwenda katika kituo husika cha Mbezi kabla ya kwenda bungeni Januari na kutoa kauli ya kutaka ndani mwezi mmoja ujenzi uwe umeanza na iwapo usingeanza nilieleza kusudio la kuunganisha nguvu ya umma baada ya kutoka bungeni mwezi Februari ili kituo hicho kianze kutumika kupunguza msongamano hata kama choo kitakuwa hakijakamilika.

Nawashukuru wananchi mlioonyesha mwamko wa kufuatilia suala hili kwa karibu na wadau wote ndani na nje ya mamlaka husika mliochukua hatua; Maslahi ya Umma Kwanza.

No comments: