Thursday, June 28, 2012

CHADEMA yalaani Dk Ulimboka kushambuliwa


CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), kimelaani kukamatwa na kushambuliwa kwa viongozi wa madaktari ikiwamo Dk Ulimboka Steven ikieleza kuwa hatua hiyo haiwezi kuwa suluhu bali itachochea zaidi mgogoro wa madaktari na Serikali.

Taarifa iliyotolewa jana na Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika inaeleza pia kwamba udhaifu wa Serikali kuharakisha kwenda mahakamani kabla ya Bunge kupewa fursa ya kujadili madai ya madaktari na kuisimamia Serikali umelifikisha taifa katika hali iliyopo sasa.

"Nalaani uamuzi wa Serikali wa kutumia vyombo vya dola kukamata na kushambulia viongozi wa madaktari ikiwemo Dk Ulimboka Steven kwa hauwezi kuwa suluhu bali utachochea zaidi mgogoro kati ya madaktari na Serikali," ilisisitiza sehemu ya taarifa hiyo ya Mnyika na kuongeza:

“Nichukue fursa hii kuwaomba madaktari kufanya kila kinachowezekana kuokoa uhai wa wagonjwa katika kipindi hiki kigumu.” Mnyika alisema kuwa ameomba wabunge wapewe nakala ya Taarifa ya Kamati ya Huduma za Jamii kuhusu madai ya madaktari na hoja ya taarifa husika iwekwe katika orodha ya shughuli za Bunge katika mkutano wa Bunge unaoendelea ili ijadiliwe na kupitisha maazimio, kuwezesha hatua za muda mfupi, wa kati na muda mrefu kuupatia ufumbuzi mgogoro huo na kuboresha sekta ya afya nchini.

“Natarajia kwamba Spika atawezesha kamati kuwasilisha taarifa yake na Bunge kujadili baada ya Serikali kutoa kauli yake bungeni,”alisema. Mnyika alisema ikiwa wabunge wataelezwa ukweli na kupewa taarifa kamili wataweza kuisimamia Serikali na kuwaeleza ukweli madaktari kipi kinawezekana na kipi hakiwezekani.

Alisema kuwa ingawa Waziri Mkuu Mizengo Pinda ametoa maelezo bungeni kuwa Serikali itatoa kauli bungeni kuhusu mgomo huo, Bunge halitaruhusiwa kujadili kauli husika, hivyo kukoseshwa fursa ya kuisimamia Serikali kwa niaba ya wananchi.

1 comment:

ALPHONCE NDONDE said...

SAFI SANA MNYIKA NA CHADEMA KWA UJUMLA WANANCHI TUPO NANYI KATIKA KUILETEA NCHI YETU MABADILIKO KATIKA NYANJA YOTE.