Monday, October 15, 2012

Mnyika: Spika aunde Kamati ya Gesi

WAZIRI Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika, amemtaka Spika wa Bunge, Anna Makinda, kutumia madaraka na mamlaka yake kutangaza kwa umma kamati nyingine ya kudumu ya Bunge itakayoshughulikia masuala ya gesi asili kabla na wakati wa mkutano wa Bunge ujao mwishoni mwa mwezi huu.

Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo kupitia CHADEMA, alisema hatua hiyo ni kutokana na hali tete na tata kuhusu sekta ndogo ya gesi asilia nchini na kwa kuzingatia umuhimu na unyeti wa sekta hiyo katika uchumi wa nchi na maisha ya wananchi.

Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Mnyika alisema pamoja na mambo mengine, Spika Makinda aelekeze kamati hiyo kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa maazimio ya Bunge ya mwaka 2011 kuhusu sekta ndogo ya gesi asili ikiwemo juu ya hatua iliyofikiwa katika kushughulikia tuhuma za ufisadi.

Madai mengine ni ya mapunjo ya fedha za mauzo ya gesi asili na hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya sera, mpango mkakati na sheria ya gesi asili.

“Hatua hii ni muhimu kufuatia ukimya wa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo kuhusu kauli yangu ya Oktoba 4, 2012 ya kutaka taarifa ya ufafanuzi kuhusu utafutaji wa mafuta na gesi asili nchini iliyotolewa na wizara hiyo Septemba 21 mwaka huu ifutwe,” alisema.

Alisema kuwa taarifa hiyo ya wizara ilieleza kuwa maandalizi ya sera ya gesi asili yapo katika hatua za mwisho wakati ambapo kamati mbalimbali za kudumu za Bunge hazijahusishwa katika mchakato huo muhimu pamoja na kuwa mamlaka ya kutunga sera kwa mfumo wa sasa ni ya Baraza la Mawaziri.

“Kwa unyeti na upekee wake sera ya gesi, Spika wa Bunge anapaswa kuwezesha Kamati za Kudumu za Bunge zihusishwe ili pawepo mashauriano na maridhiano kwa mapana na marefu,” alisema.

Mnyika alisema izingatiwe kwamba katika mkutano wa nane wa Bunge, Spika alitangaza kuwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imevunjwa na kwamba majukumu iliyokuwa ikishughulikiwa yatashughulikiwa na kamati nyingine kwa mujibu wa madaraka na mamlaka ya spika.

Chanzo: http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=41561

No comments: