Wednesday, July 17, 2013

Kodi ya kadi ya simu (SimcardTax): Maoni ya awali ya wananchi juu ya hatua za kuchukuliwa

Nawashukuru kwa maoni ambayo mmenitumia kuhusu hatua zinazopaswa kuchukuliwa kufuatia kuanzishwa kwa ushuru wa bidhaa kwa kadi za simu (sim card) kwa wamiliki wa simu za kiganjani/mkononi.

Bado naendelea kuchambua maelfu ya maoni yaliyotolewa katika mijadala na niliyotumiwa kwa barua pepe. Nitoe mrejesho wa awali kwamba kwa muktasari mapendekezo niliyoyachambua mpaka sasa yanapendekeza hatua zifuatazo kuchukuliwa:


Kwanza, taarifa itolewe kwa wanahabari na umma yaliyojiri na yatokanayo na kupitishwa kwa kodi hiyo;

Pili, hatua zisiwe kwa kodi hii pekee yake bali zote zenye kuongeza gharama za maisha kwa wananchi.

Tatu; majina ya wabunge wanaodaiwa kutoa mawazo ya kupendekeza kodi hiyo kutozwa yatajwe;

Nne, muswada wa sheria upelekwe bungeni katika mkutano ujao kufuta kodi hiyo;

Tano, saini za wananchi zikusanywe kupinga kodi hiyo na kuwasilishwa bungeni au kwa Serikali;

Sita, Serikali itakiwe kusitisha utekelezaji wa kifungu husika cha sheria hiyo ili wananchi wasianze kubebeshwa mzigo huo wa gharama;

Saba, maandamano yaandaliwe kulaani kupitishwa kwa kodi hiyo na kutaka utozaji wa kodi hiyo usianze kutekelezwa;

Hatua ambazo tayari zimeanza kuchukuliwa:

Wakati nikiendelea na uchambuzi nimeanza pia kuchukua hatua namba moja mpaka tano. Nashukuru pia kwa upande wenu baadhi mmeanza kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kukusanya saini kupitia link hii: http://www.avaaz.org/en/petition/WITO_WA_KUSITISHA_TOZOKODI_YA_LAINI_YA_SIMU_KILA_MWEZI_KUFUATIA_MABADILIKO_YA_SHERIA_YA_KODI_2013/?aCqNffb Naunga mkono hatua hiyo iliyochukuliwa na nawahimiza wengine kuingia na kusaini.

Aidha, natoa mwito kwa kila mwananchi aliyeguswa na suala hili kwa kutumia haki yake kwa kuzingatia wajibu muhimu kuwezesha hatua mbalimbali kuchukuliwa kwa kurejea mapendekezo yaliyotolewa.

Kwa upande wangu; Mosi, kupitia mkutano wa hadhara tarehe 13 Julai 2013 na njia nyingine niliendelea na mchakato ulionza kabla ya mkutano wa kumi na moja wa Bunge kuanza wa kukusanya saini za watu wanaotoa madai ya kutaka Bunge liisimamie Serikali kupunguza athari za ongezeko la gharama za maisha kwa wananchi na kudhibiti mfumuko wa bei nchini. Mpaka sasa zimeshafika saini 23569. 

Yeyote anayetaka kukusanya saini za wengine katika eneo lake naomba awasiliane na Afisa katika ofisi ya mbunge Gaston Garubimbi (0715/0767-825025) kwa ajili ya kutumiwa fomu.

Aidha, nitashiriki mkutano wa hadhara jumapili tarehe 21 Julai 2013 katika Uwanja wa Sahara kata ya Mabibo kuanzia saa 8 Mchana mpaka saa 11 Jioni. Hivyo, kwa wale mlio katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar Es Salaam mnaalikwa kuhudhuria mkutano huo ambapo mtapata pia fursa ya kusaini fomu tajwa.

Mkutano huo unalengo la kutoa mrejesho kuhusu yaliyojiri bungeni katika mkutano uliopita na kupokea masuala ya kuyawasilisha katika mkutano ujao. Aidha, uchambuzi utafanyika kuhusu rasimu ya katiba sanjari na juu ya mchakato wa katiba mpya. 

Pili, tarehe 15 Julai 2013 niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge kusudio la kuwasilisha muswada binafsi wa sheria kuwezesha kufutwa kwa ushuru tajwa. Katika barua hiyo nimeomba masharti ya kanuni ya Kanuni ya 21(1) (d) (e) na (2) ya Kanuni za Kudumu za Bunge yazingatiwe kuniwezesha kuchukua hatua hiyo katika Mkutano wa kumi na mbili wa Bunge uliopangwa kuanza mwezi Agosti 2013. Hivyo, yeyote ambaye angependa kujitolea 3M (Maarifa, Muda au Mali) kufanikisha maandalizi ya muswada huo awasiliane nasi kupitia barua pepe mbungeubungo@gmail.com. Maslahi ya umma Kwanza.


John Mnyika (Mb)

18 Julai 2013

4 comments:

Unknown said...

https://www.facebook.com/groups/473092632784438/

Anonymous said...

Big up kijana, kwa kujitoa mwanga katika kutetea maslai ya umma kwa serikali dhalimu,haramu ya ccm. Tuko nyuma yako usiogope kiongozi; hakuna mamlaka iliyo juu zaidi ya nguvu ya umma ilioko nyuma yako. Binafsi nimeshatia sign yangu kupinga tozo za line za cm, kupitia link hiyo hapo juu.

Anonymous said...

Tupo pamoja mkuu. Ila nawaomba kunapotokwa kujadili mambo ya msingi kama haya bungeni msiwaache wabunge wa ccm peke yao. Tunajua wakati wa kupitisha haya nyie wabunge wawanawanchi hamkuwapo sasa next time mjigawe wengine wabaki bungeni manake mkiwaacha hawa jamaa wanapitisha kla kitu bila kujali vina madhara gani kwa wapuga kura wao. Ona mliwaachia bucha fisi wamemaliza nyama.

Anonymous said...

Hongera sana Mh. Mbunge wetu. Kodi hii na ukandamizaji mwingine wowote ule unaofanywa na serikali hii dhalimu sharti ukomeshwe Kwa njia zozote zile. Naunga mkono kusudio hili maana Lina Mungu ndani yake. Ujaliwe nguvu na maarifa zaidi katika kutuongoza kufikia mabadiliko kamili.