Sunday, February 23, 2014

TAARIFA KWA UMMA: SAKATA LA FIDIA YA ENEO LA MLOGANZILA

Mbunge wa Jimbo la Ubungo, John Mnyika ameendelea kufuatilia kuhusu fidia ya ardhi ya wananchi wa kata ya Kwembe waliohamishwa baada ya kulipwa fidia ya maendelezo pekee kupitisha ujenzi wa Chuo Kikuu cha Muhimbili (MUHAS) kampasi ya Mloganzila.

Kwa upande mwingine, Mbunge Mnyika ameendelea pia kuhoji katika mamlaka mbalimbali juu ya kauli za viongozi wa Serikali kutamka kwamba eneo hilo lipo katika Mkoa wa Pwani badala ya Manispaa ya Kinondoni jijini Dar Es Salaam.

Tarehe 19 Januari 2014 Mbunge Mnyika alifika katika kata ya Kwembe na kukutana na wananchi kusikiliza malalamiko yao na mara baada ya mkutano huo alizikutanisha kamati mbili zinazofuatilia suala hilo.

Kufuatia hatua hiyo, Mbunge Mnyika aliwasiliana na Waziri Mkuu Mizengo Pinda na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuwakumbusha kutekeleza ahadi zao za kuupatia ufumbuzi mgogoro huo kufuatia hatua ya mbunge kuhoji suala hilo bungeni kwa nyakati mbalimbali kati ya mwaka 2011 mpaka 2013. (Baadhi ya rejea kutoka Kumbukumbu Rasmi za Bunge-Hansard zimeambatanishwa).

Ofisi ya Mbunge inalazimika kutoa taarifa hii kwa umma kwa kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi zimeshindwa kutimiza wajibu wa kutoa majibu ya barua hata baada ya ofisi ya mbunge Jimbo la Ubungo kwenda katika ofisi zao mara kwa mara kufuatilia suala hilo.

Kutokana na hali hiyo, Mbunge Mnyika amechukua uamuzi wa kumshauri Rais Jakaya Kikwete kuingilia kati na kutoa kauli kwa umma kuhusu fidia ya ardhi kwa wananchi hao. Rais awezeshe kutekelezwa kwa ahadi ya kuwapatia shilingi milioni 9 za fidia ya ardhi au viwanja mbadala kama ilivyoahidiwa kwa nyakati mbalimbali kati ya mwaka 2009 na 2010.

Itakumbukwa kwamba tarehe 11 Disemba 2012 Rais Kikwete katika hotuba yake ya uzinduzi wa jengo la huduma za mama na mtoto katika hospitali ya Sinza, Rais alitoa maelezo yasiyokuwa sahihi kwamba wananchi wameshalipwa fidia zote ila wanadai fedha za ziada za usumbufu kutokana na kuchochewa na wapinzani.

Tarehe 12 Disemba 2012 Mbunge Mnyika alieleza umma kwamba Rais alipotoshwa kuhusu suala hilo na kwamba malipo ya fidia kwa wananchi bado hayajakamilika na  kukumbusha kwamba ahadi za kutoa fidia hizo haikutolewa na  upinzani bali Serikali kupitia kwa aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi John Chiligati na aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Patrick Rutabanzibwa.

Kadhalika kamati ya wananchi nayo iliandika barua kwa Rais yenye maelezo na vielelezo juu ya madai ya msingi ya wananchi ambayo tangu mwaka 2013 mwanzoni mpaka sasa haijapatiwa majibu na ikulu hivyo ni wakati muafaka sasa wa Rais Kikwete mwenyewe kufuatilia na kuagiza hatua kuchukuliwa kwa manufaa ya wananchi.

Ofisi ya Mbunge inasisiza kwamba Mnyika au kamati za wananchi au mtu mwingine yeyote anapofuatilia suala hili isionekane kuwa ni uchochezi bali ni sehemu ya uwakilishi na uwajibikaji kuwezesha haki kutendeka na miradi ya maendeleo kutekelezeka kwa ufanisi.

Imetolewa tarehe 22 Februari 2014 na:
Aziz Himbuka
Katibu Msaidizi

Ofisi ya Mbunge

VIELEZO VYA KUREJEA:
Mnyika bungeni kuhusu Mloganzila-14 Agosti 2012




Rejea ya Mloganzila-Majibu ya Serikali bungeni kufuatia maswali ya Mnyika



No comments: